Mwanasiasa na mwanauchumi mashuhuri, Bwana Waita Nzioka, ametangaza kwa msisitizo kuwa uamuzi kuhusu uongozi wa Kaunti ya Machakos mwaka 2027 uko mikononi mwa wakazi na wapiga kura wa kaunti hiyo. Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika mjini Machakos, Waita alisisitiza kuwa ni wananchi wenyewe wanaopaswa kuamua hatma ya maendeleo ya kaunti yao.
“Nina imani kuwa wakazi wa Machakos wana uwezo na hekima ya kufanya maamuzi sahihi kuhusu mustakabali wa kaunti hii. Uongozi haupaswi kuamuliwa na makundi ya kifisadi au maslahi ya watu wachache. Ni kura ya mwananchi wa kawaida ndiyo itakayoamua,” alisema Waita.
Waita Nzioka, ambaye aligombea nafasi ya Ugavana wa Machakos mwaka 2022 lakini hakufanikiwa, ameweka wazi nia yake ya kuwania tena kiti hicho katika uchaguzi mkuu wa 2027 kupitia kampeni yake mpya inayojulikana kama #MasakuMbee2027.
Katika hotuba yake, alieleza ajenda yake kuu kuwa ni kuimarisha huduma za afya, kuboresha miundombinu, na kuinua uchumi wa kijiji kupitia uwekezaji katika sekta ya kilimo na biashara ndogondogo.
Aliwataka wananchi kuwa waangalifu na viongozi wanaowapa ahadi zisizotekelezeka na badala yake wachague viongozi wanaoweka mbele maslahi ya watu.
Uwaniaji wake umeongeza msisimko wa kisiasa katika Kaunti ya Machakos, huku wananchi wakisubiri kuona mikakati atakayoweka mbele kuelekea uchaguzi wa 2027.
Mwisho







